Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Wednesday, April 1, 2015

MIAKA MIWILI YA AMKA MTANZANIA; Kwa Nini Ipo Na Itaendelea Kuwepo Na Mambo Mazuri Yanayokuja.

Tarehe 31/03/2013 ilikuwa ndio siku ya kwanza kwa makala ya kwanza kwenda hewani kwenye mtandao huu wa AMKA MTANZANIA. Kipindi hiko wakati naanzisha mtandao huu mambo hayakuwa kama sasa, watu walikuwa na muamko mdogo wa kusoma habari za aina hii na hata kujisomea vitabu. Leo hii miaka miwili tu mbele, mambo yamebadilika kwa kiasi kikubwa sana

Leo hii, miaka miwili baadaya kuanzishwa kwa mtandao huu nimeona ni vyema tukashirikishana kwa nini mtandao huu upo, utaendelea kuwepo na mambo makubwa yanayokuja.

Moja ya makala za mwanzo kabisa kwenye AMKA MTANZANIA;

UTARATIBU WA KUJISOMEA VITABU

USIMLAUMU YEYOTE, ANZA KUJILAUMU WEWE

ZOEZI ZURI LA KUFANYA KILA SIKU

Kwa nini mtandao huu upo?

Miaka miwili kabla ya kuanz akwa mtandao huu, nilikuwa naishi kwenye hadithi nzuri ambayo tumekuwa tukidanganywa. Hadithi kwamba nenda shule, soma kwa bidii, faulu vizuri na utapata kazi nzuri na kuwa na maisha mazuri. Nilisoma kwa bidii kweli na kufaulu vizuri sana masomo yangu ya kidato cha sita. Baada ya hapo nilipata nafasi ya kusomea udaktari wa binadamu. Kwa nafasi hii niliamini ndio nimepata tiketi ya maisha mazuri.

Lakini mambo yalibadilika sana baadaya ya kuanza masomo haya ya udaktari. Baada ya kuona kile nitakachokwenda kufanya na mazingira ya kukifanya na hata maisha ya madaktari wengine, sikushawishika sana kama mwanzo kwamba kuwa daktari ndio tiketi ya maisha bora.

Changamoto kubwa zaidi ilitokea mwaka 2011 ambapo nilijikuta nje ya mfumo wa elimu, huku sina degree wala chochote cha kuniwezesha kupata kazi ya kujikimu kwenye maisha yangu. Mbaya zaidi hakuna aliyeweza kunielewa kwenye kipindi hiki kwa sababu kila mtu anayenifahamu aliona nimefanya makosa makubwa sana kwenye maisha, sijui ninachofanya na mengine mengi. Ni hapa ndio nilipoamua kushika hatamu ya maisha yangu. Nilikaa chini na kuamua kwamba kama nitakwenda kufanikiwa kwenye maisha yangu, basi hiyo ni juu yangu. Na nilijiambia kabisa kwamba mafanikio kwenye maisha hayahitaji degree au elimu yoyote kubwa.

Ni baada ya maamuzi haya ndipo niliacha kulalamika na kuanz akuchukua hatua juu ya maisha yangu. Nilitafuta kazi yoyote ninayoweza kufanya ili angalau iniwezeshe kuendelea kuwepo mjini. Nilipata kazi hiyo na sio kwa sababu ya kuwa nimesomea kazi hiyo, au kwa sababu ya kujulikana, bali kwa ushawishi niliokuwa nautoa kwenye maombi ya kazi hiyo.

Baada ya hapa niliamua kujifunza na kuangalia ni kitu gani ninachopendelea kufanya. Nilianza kujifunza mambo yanayohusiana na teknolojia ya habari(IT) ambapo nilijifunza jinsi ya kutengeneza tovuti, blog, programu za kompyuta na vitu vingine vingi. Yote haya sikuwa na darasa la kufundishwa, bali nilitafuta vitabu na kujisomea kisha kufanyia kazi yale ambayo nimeyasoma. Uzuri ni kwamba nilikuwa naona matokeo mazuri kila ninapojifunza na kufanya kitu.

Baada ya mwaka mmoja wa kujifunza vitu vya kitaalamu na pia kujisomea vitabu vyakujijenga na kujihamasisha niliona mabadiliko makubwa sana kwenye maisha yangu. Kwanza nilijikuta katika hali kubwa ya kujiamini, nikiwa na vyanzo mbalimbali vya mapato kutoka kwenye shughuli mbalimbali ambazo nilikuwa naweza kufanya. Ni katika wakati huu ambapo niliona makosa makubwa niliyokuwa nafanya kwenye maisha yangu na jinsi nilivyoweza kuyarekebisha.

Ni wakati huu pia ambapo niliona watu wengi wanafanya makosa haya na kunafanya maisha yao yawe magumu sana. Ndio maana niliona kuna umuhimu wa kuwashirikisha vitu hivi vizuri ambavyo nimefanya kwenye maisha yangu na ninaendelea kuvifanya ili nao waweze kuboresha maisha yao. Hapa ndipo mtandao huu wa AMKA MTANZANIA ulipozaliwa. Lengo kubwa la mtandao huu ni kumsaidia kila mtanzania ambaye ameamua kushika hatamu ya maisha yake kuweza kufikia malengo na mipango aliyojiwekea kwenye maisha yake.

Kwa nini nimekushirikisha sehemu hiyo ndogo ya maisha yangu na historia ya mtandao huu?

Nimefanya hivi kwa sababu najua kuna kijana wa kitanzania ambaye amemaliza masomo yake ila hajapata ajira. Kijana huyu amekaa nyumbani na hajui afanye nini, kwani hata biashara anasema hana mtaji. Nataka kukuambia wewe kijana mwenzangu kwamba AMKA na uchukue hatamu ya maisha yako, utakapoamua kuamka hakuna linaoshindikana.

Najua kuna mfanyakazi ambaye amefanya kazi kwa muda mrefu sasa ila haoni kitu kikubwa ambacho amefanya kwenye maisha yake. Maisha yake yamekuwa ya kuamka, kwenda kazini, kurudi nyumbani na kesho pia kufanya hivyo. Kipato anachopata pia hakioni kwa sababu kinaishia kulipa madeni na kulipia gharama za maisha. Nataka kukuambia wewe mtanzania mwenzangu, haijalishi kazi yako ni ya chini kiasi gani, haijalishi umeifanya kw amuda gani, kuna njia nzuri sana za wewe kuweza kuyabadili maisha yako na kuwa bora sana zaidi ya sasa ambapo unayaona yanakwenda tu.

Pia najua kuna mfanyabiashara ambaye amekuwa anafanya biashara zake kwa muda mrefu ila haoni mabadiliko yoyote kwenye biashara hiyo. Au ameanza biashara na kupata hasara hivyo kuamini kwmaba biashara haiwezekani. Napenda kukuambia kwamba kuna mbinu nzuri sana za kufanya biashara zako na kama ukiamua kuzitafuta na kuzifuata maisha yako yatakuwa tofauti sana na yalivyo sasa.

Maisha yoyote ambayo unapitia sasa, hata yawe magumu kiasi gani, unayo nafasi kubwa sana ya kuyabadili wewe mwenyewe. Huna haja ya kulaumu serikali, kulaumu wazazi au kulaumu mtu mwingine yeyote unayefikiri ndio anakuletea maisha hayo magumu. Leo nakuambia kwamba, maisha magumu uliyonayo, yataondolewa na wewe mwenyewe.

Kwa nini AMKA MTANZANIA itaendelea kuwepo.

AMKA MTANZANIA itaendelea kuwepo kwa sababu bado watanzania wengi hawajaamka. Bado watanzania wengi wamekabidhi maisha yao kwa waajiri wao, kwa serikali, kwa jamii na wameruhusu taasisi hizi zifanye maamuzi muhimu kwenye maisha yao. Hii ndio maana wanaona maisha yao yakienda tu na hivyo kuishia kulaumu pale ambapo kile walichotarajia hakijatokea.

Bado watanzania tunahitaji maarifa muhimu sana ya kuweza kuboresha maisha yetu na kufanikiwa zaidi. Sehemu kubwa sana ya watanzania wanafanya mambo kwa mazoea. Wanafanya kazi kwa sababu ndio kazi ambayo wamekuwa wanaifanya kila siku. Wanafanya biashara kwa sababu wamezoea kufanya biashara hiyo. Hii ni sumu kubwa sana ya kufikia mafanikio makubwa kama unavyoweza kuisoma vizuri kwenye kitabu JINSI YA KUFAIDIKA NA MABADILIKO YANAYOTOKEA.

Mtandao huu utaendelea kuwepo na kutoa makala na mafunzo mazuri yatakayomwezesha kila aliyeamua kuboresha maisha yake kuweza kufikia lengo hilo.

Mambo mazuri yanayokuja kwenye AMKA CONSULTANTS.

Ilianza AMKA MTANZANIA ambayo ilikuwa na jukumu kubwa la kukupa wewe taarifa muhimu unazohitaji kuwa nazo ili kuboresha maisha yako. Mwaka mmoja baadae ikaja KISIMA CHA MAARIFA ambayo ni sehemu maalumu kwa wale ambao wako tayari kufikia mafanikio makubwa sana kwenye maisha yao. Kupitia KISIMA CHA MAARIFA watu wanajifunza tabia za mafanikio, mbinu za kufikia mafanikio, biashara na ujasiriamali na hata kupata uchambuzi wa vitabu vizuri. Kupitia KISIMA CHA MAARIFA pia unapata nafasi ya kukutana na watanzania wengine ambao nao wanaelekea kwenye safari ya mafanikio.

Kuna mambo mengi na mazuri ambayo yataendele akukujia kupitia mtandao huu wa AMKA MTANZANIA na KISIMA CHA MAARIFA. Endelea kutembelea mitandao hii na washirikishe wengi zaidi ili nao wapate mambo haya mazuri.

Kuna kipengele muhimu kitakachokuja kwenye AMKA MTANZANI ambapo tutapata shuhuda za watu mbalimbali ambao maisha yao yamebadilika sana baada ya kujifunza kupitia AMKA MTANZANIA na kuamua kufanyia kazi yale ambayo wamejifunza. Shuhuda zipo nyingi mpaka sasa. Kama na wewe ungependa kuwashirikisha watanzania wenzako ushuhuda mzuri kutokana na uliyojifunza kwenye mtandao huu tafadhali andika maelezo yako kwa kujitambulisha, kueleza ulipotoka, ulipo sana na unapokwenda na jinsi gani AMKA MTANZANIA imekusaidia kisha tuma kwenye email makirita@kisimachamaarifa.co.tz Tafadhali fanya hivi na utakuwa sehemu ya mabadiliko ya nchi yetu na watanzania wenzetu.

Ufanye nini ili maisha yako kuwa bora ziadi?

Kwanza kabisa chukua maamuzi juu ya maisha yako, jua kama utakwenda kufanikiwa basi ni kwa juhudi zako na hakuna atakayekuletea mafanikio hayo.

Pili amua kujifunza sana kuhusiana na hiko unachofanya na maisha yako kwa ujumla. Jisomee vitabu mbalimbali vinavyotumwa kwenye mtandao huu na endelea kusoma mtandao huu kila siku kwa sababu kila siku kunakuwa na makala nzuri za kukuwezesha kuboresha maisha yako.

Tatu, jiunge na KISIMA CHA MAARIFA, kwa kuwa ndani ya kisima utajifunza mbinu nyingi sana za kukuwezesha kufikia mafanikio na pia utapata nafasi ya kukutana na watanzania wengine ambao wameamua kuchukua hatamu ya maisha yao. Bonyeza maandishi haya kujiunga na KISIMA CHA MAARIFA na weka taarifa zako kisha lipa ada ya uanachama na utapata nafsi ya kupata maarifa hayo adimu. Kuhakikisha unapata mambo yote mazuri lipia ada ya GOLD MEMBER.

Naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana wewe msomaji ambaye umekuwa na mtandao huu mpaka sasa. Ni kwa sababu yako ndio maana mtandao huu umeendelea kukua na kuwafikia wengi zaidi. Umekuwa ukiwashiriksiha wengine habari za mtandao huu na kuwafanya wautembelee pia. Tafadhali endelea kuw abalozi mzuri wa AMKA MTANZANIA na hakikisha kila mtu unayemfahamu naye amefahamu kuhusu mtandao huu ili na yeye autembelee na kujifunza.

Pia niseme kwamba sisi sote tunaendelea na safari ya kujifunza, hakuna anayejua zaidi bali tunajifunza na wakati mwingine tunafanya makosa. Mimi na waandishi wengine wa mtandao huu sio kwamba ndio mabingwa sana kwenye kile tunachoandika, ila tunapenda kujifunz ana kutumia mambo haya na maisha yetu yanakuwa bora zaidi kadiri siku zinavyokwenda. Na wewe usikose nafasi hii ya kuboresha maisha yako kila siku hata kama ni kidogo kiasi gani.

Nakutakia kila la kheri katika kuboresha maisha yako. Kumbuka kwamba kila kitu kinawezekana kama ukiamua kuchukua hatua. Kama kuna jambo lolote ambalo linakupa changamoto na ungependa kupata ushauri zaidi karibu sana tuwasiliane. Unaweza kupiga simu kwenye namba 0717396253 na tukaona ni jinsi gani tunaweza kusaidiana kwenye jambo hilo.

TULIKUWA PAMOJA, TUPO PAMOJA NA TUTAENDELEA KUWA PAMOJA. Tafadhali tuma makala hii kwa njia ya email kwa watu watano na nicopy(weka email yangu makirita@kisimachamaarifa.co.tz kwenye sehemu ya cc) kwenye email hiyo na nitakutumia zawadi nzuri ya kitabu cha kufaidika na mabadiliko.

kitabu-kava-tangazo4322

Tafadhali Washirikishe Wengine Makala Hii Nzuri!
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →
Powered By: BloggerYard.Com

0 comments:

Post a Comment