Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Showing posts with label RAIS KIVULI. Show all posts
Showing posts with label RAIS KIVULI. Show all posts

Thursday, January 1, 2015

Salamu Za Mwaka Mpya Kutoka Kwa Rais Wa Tanzania Mwaka 2040.

Napenda kuchukua nafasi hii ya kipekee kuwatakia watanzania wenzangu wote kheri na hongera ya kuuona mwaka 2015. Sio watu wote walioanza mwaka 2014 wamepata nafasi ya kuuona mwaka 2015, hivyo ni jambo la kushukuru kwa nafasi hii ya kipekee.

Mwaka 2014 huenda ulikuwa mwaka uliokuwezesha kufanikisha mengi na pia kushindwa mengi. Kikubwa cha kuchukua 2014 na kukileta mwaka 2015 na yale uliyojifunza. Katika kila jambo ulilofanikiwa kuna vitu umejifunza na katika kila jambo uliloshindwa kuna vitu vingi umejifunza. Tumia yote uliyojifunza ili mwaka 2015 uwe bora zaidi kwako.

Kama mwaka 2014 kuna vitu ulipanga kufanikisha ukashindwa, hii ina maana kwamba kuna vitu unafanya kwa makosa au kuna vitu hufanyi kabisa. Hivyo kuendelea hivyo hivyo kwa mwaka 2015 utapata majibu yale yale uliyopata mwaka 2014. Kumbuka ujinga ni kufanya jambo lile lile kwa njia ile ile na kutegemea majibu tofauti. Haiwezekani na utazidi kupoteza muda wako.

Mwaka huu 2015 ni mwaka ambao utakuwa na matukio mengi na makubwa kitaifa. Matukio haya mengi yatakuwa chachu muhimu katika maendeleo ya nchi yetu. Mambo mawili makubwa kabisa yatakuwa;

1. Kupigia kura katiba pendekezwa. Sote tunajua katiba ilivyo muhimu kwenye taifa lolote, hivyo tukio la kupigia kura katiba iliyopendekezwa ni tukio muhimu sana.

2. Uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani. Mwaka huu tutapata nafasi ya kuchagua viongozi watakaofanya maamuzi kwa niaba yetu kwa miaka mitano ijayo. Hivyo ni jambo linalohitaji umakini wetu ili tusijekupata viongozi ambao watafanya taifa likose uelekeo.

Matukio haya mawili na mengine yatakayotokea mwaka huu 2015 yameshika hisia za wananchi wengi. Wananchi wengi tunaamini mabadiliko makubwa sana kwenye maisha yetu yatatokea baada ya kupata katiba mpya na kufanya uchaguzi mkuu. Natoa tahadhari kwamba tusitegemee sana hili, mabadiliko ya kweli yanaanzia ndani yako wewe mwananchi. Kila mwananchi anatakiwa kubadilika ndio taifa liweze kubadilika. Kila mwananchi anatakiwa kupata maendeleo ndio taifa lipate maendeleo. Na kwa bahati mbaya sana sehemu kubwa ya mabadiliko ya nchi haitokani na kile serikali inachofanya, bali kile ambacho kila mwananchi anafanya.

Kitu kingine kikubwa ninachopenda kukigusia kwenye salamu hizi za mwaka mpya ni matatizo mawili makubwa yanayoturudisha nyuma kama taifa. Matatizo haya yamekuwa ndio chanzo cha uzembe na ufisadi mkubwa unaoendelea kwenye nchi hii kwa sasa. Matatizo hayo ni;

1. Kutokufanya kazi kwa bidii na maarifa. Najua watanzania tunachukia sana pale tunapoambiwa sisi ni wavivu, ila hata tukichukia huo ndio ukweli wenyewe. Sehemu kubwa ya wananchi ni wavivu au hawafanya kazi kwa viwango ambavyo wanategemewa kufanya. Kila mtu anatafuta njia rahisi ya kupata fedha. Kila mtu anataka apate kitu pasi na kutoa kitu. Hatimaye hii imetuletea wizi na ufisadi mkubwa kwenye taifa. Najua nikisema ufisadi utakimbilia kwenye ESCROW na EPA, lakini je vipi kuhusu daktari anayetaka rushwa ili amhudumie mgonjwa?

Vipi kuhusu afisa wa kodi TRA anayetaka rushwa ili kumsaidia mtu asilipe kodi stahiki?

Vipi kuhusu mwenyekiti wa serikali ya mtaa anayetaka shilingi elfu mbili ndio akupe barua ya utambulisho?

Vipi kuhusu muuza maziwa anayeweka maji kwenye maziwa ili apate zaidi?

Vipi kuhusu kondakta anayepandisha nauli kwa sababu tu kuna watu wengi wanaotaka kusafiri na usafiri ni wa shida?

Vipi kuhusu mwalimu aliyepangiwa kituo cha kazi ila haonekani kazini?

Vipi kuhusu askari wa usalama barabarani anayetaka rushwa kuruhusu gari ambalo halina sifa za kuwepo barabarani kuendelea na safari? Na baadae lisababishe ajali?

Tukiangalia matukio yote haya tunaona ni jinsi gani sehemu kubwa ya taifa tumemezwa na vitendo vya wizi na ufisadi. Tunapiga kelele kukemea ufisadi mkubwa lakini sisi sisi ndio wa kwanza kufurahia kutoa rushwa ili tupate huduma tunazozitaka kwa haraka.

2. Tatizo la pili ni uadilifu, hili ndio linatumaliza kama taifa na ndio linazaa tatizo na kwanza la kutokufanya kazi kwa bidii na maarifa na hatimaye kujiingiza kwenye wizi na ufisadi.

Ni lazima sisi kama wananchi tuanze kujimulika wenyewe, tuone je matendo tunayofanya kila siku kama yangefanywa kuwa ndio sheria ya nchi nzima nchi yetu ingefika wapi?

Tunakuwa wepesi kuwalaumu viongozi kwa tabia zao mbaya lakini tunasahau viongozi hawa wametoka katikati yetu sisi na hivyo wanapeleka tabia walizokuwa nazo kwenye ngazi za juu zaidi.

Kwa hayo machache nikutakia mwaka mzuri na wenye mafanikio makubwa. Nakusihi sana mwaka huu simamia nguzo hizi tatu muhimu

1. Kufanya kazi kwa bidii na maarifa.

2. Kuwa mwaminifu, tekeleza kile unachoahidi.

3. Kuwa muadilifu, usimfanyie mwingine kile usichopenda kufanyiwa.

Mwaka huu 2015 AMKA CONSULTANTS imejipanga vizuri ili kufanya kazi na wewe na uweze kuboresha maisha yako na kufikia mafanikio makubwa.

Kila siku tembelea AMKA MTANZANIA ili kujifunza na kuhamasika na uweze kuboresha maisha yako.

Tembelea na ujiunge na KISIMA CHA MAARIFA ambapo utakutana na jumuiya ya watu ambao wamechoka kuwa wa kawaida na wanataka kufanya na kuwa zaidi ya walivyo sasa.

Pia tembelea blog hii MAKIRITA AMANI ambapo utakuwa unapata chakula cha ubongo, mambo ambayo yatakufanya ufikiri zaidi na kukuhamasisha kuchukua hatua kwenye maisha yako.

Pata picha hii, leo umekabidhiwa kitabu kitupu kabisa chenye kurasa 365 na unaamua uandike nini kwenye kila ukurasa, je ukurasa wa leo umeandika nini? Na wa kesho je?

Mwaka 2015 ukawe mwaka wa mafanikio makubwa kwako.

TUPO PAMOJA.

Makirita Amani,

Rais wa Tanzania mwaka 2040.

Sunday, December 14, 2014

Nenda Kapige Kura, Au Usipige Na Fanya Hivi…

Leo ni siku ya kupiga kura kuwachagua viongozi wa serikali za mitaa, najua unajua hili, ila imebidi niliandike tena ili tupate pa kuanzia. Kama ulikuwa hujui leo ndio siku ya uchaguzi basi tuna tatizo kubwa zaidi.

Kwa takwimu mbalimbali za chaguzi zilizopita tunaona idadi kubwa ya watu waliojiandikisha hawapigi kura. Na laiti kama watu hao wangepiga kura mabadiliko yangekuwa makubwa sana.

kupiga kura

Sasa sitaki kuandika mengi nikucheleweshe kupiga kura, ninachokuambia leo ni;

Nenda kapige kura, au usiende kupiga na usilalamike chochote.

Maana watanzania tumekuwa mafundi wa kulalamika ila hatua hatuchukui. Kama hatua kubwa za kuwawajibisha watu hatuwezi kuchukua, basi tuchukue hatua ya kupiga kura na kuchagua viongozi ambao ni bora.

Wahi kapige kura yako asubuhi hii, na mhamasishe kila unayekutana naye nae akapige kura.

Hapa ndipo mabadiliko ya nchi yetu yanapoanzia.

Monday, November 3, 2014

Tukemee Tabia Hii Mbaya Kama Taifa.

Jana tarehe 02/11/2014 kulikuwa na mdahalo wa katiba ulioandaliwa na taasisi ya Mwalimu Nyerere uliokuwa unafanyika katika ukumbi wa ukumbi wa ubungo plaza.

Katika mdahalo huo waliokuwa wajumbe wa iliyokuwa tume ya katiba walialikwa kuzungumza na baadae wananchi waliohudhuria nao wangepata nafasi ya kuzungumzia katiba pendekezwa.

Lengo kubwa la mdahalo huo na mingine ambayo tuliahidiwa itafuata ilikuwa kuwapa uelewa wananchi juu ya katiba pendekezwa kabla wakati wa kupiga kura haujafika.

Binafsi ninaona kitu hiki ni kizuri sana maana taasisi inayoandaa midahalo hii haina uegemeo wowote wa kisiasa na hivyo itatoa nafasi nzuri ya wananchi kujifunza yaliyomo kwenye katiba pendekezwa.

Katika hali ya kushangaza wakati mdahalo unaendelea na Jaji Warioba akizungumza kiliibuka kikundi cha watu ambao walionesha mabango ya kupinga mdahalo ule na kusema kwamba wanaikubali katiba pendekezwa. Hata walipotakiwa kutulia chini ili mdahalo uweze kuendelea bado hawakusikia na hatimaye ikapelekea vurugu kubwa na mdahalo kuahirishwa.

WARIOBA

Kwanza kabisa hiki ni kitendo cha ajabu sana ambacho kinatakiw akulaaniwa na kila Mtanzania ambaye ana mapenzi mema na nchi hii. Ni kweli kabisa hatuwezi kukubaliana wote, ila kutofautiana kwetu kifikra na kihoja kusifanye tuonanae kama maadui. Hizi ni siasa chafu na za kitoto sana ambazo naona zinanyamaziwa na wanaofanya ujinga huu wanaonekana kama wanaleta manufaa kwa kikundi fulani.

Kama unaona mtu anakushinda kwa hoja njia sahihi ni kuleta fujo na kupigana? Hapana hii sio njia sahihi kabisa na kama tutaendelea kuacha mambo haya yaendelee tutalipeleka taifa kubaya.

Katiba ni kitu ambacho kinamhusu kila mwananchi na hivyo kila mwananchi ana uhuru wa kutoa maoni yake na hisia zake juu ya katiba hii. Lakini katika kutoa maoni hayo na hisia hizo usiingilie uhuru wa mwenzako au kuleta fujo au kumwona anayeamini tofauti na wewe ni adui.

Naomba watanzania wote tulaani kitendo hiki kilichotokea na tusitoe tena nafasi ya kutokea kwa kitendo kama hiki.

Tanzania ni nchi yetu sote, tushirikiane kuijenga.

TUPO PAMOJA.

Sunday, November 2, 2014

Uchaguzi Wa Serikali Za Mitaa Ni Muhimu Sana. Tuzingatie Mambo Haya Matano.

Tarehe 14/12/2014 itakuwa siku muhimu sana katika miaka mitano ijayo. Siku hii itakuwa ni siku ya uchaguzi wa serikali za mitaa. Watu wengi sana hawaupi uchaguzi huu nafasi kubwa na wameelekeza macho na masikio yao kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Hili ni kosa kubwa sana ambalo tunafanya watanzania wenzangu. Uchaguzi wa serikali za mitaa ni muhimu kama ilivyo uchaguzi mkuu. Ni kupitia serikali za mitaa ambapo tunakuwa na demokrasia ya moja kwamoja. Yaani kama kuna jambo lolote la kufanya maamuzi kwenye mtaa au kijiji basi wananchi wote watafanya maamuzi kwenye vikao na mikutano mbalimbali.

Pia serikali hizi za mitaa zina mamlaka ya kutunga sheria ndogo ndogo ambazo zinaweza kuwa na athari chanya au hasi kwetu sisi wananchi.

Serikali za vijiji zina mamlaka makubwa sana kwenye ardhi na hivyo zinaweza kufanya maamuzi ya kuuza ardhi kwa watu mbalimbali. Hivyo unapokuwa na serikali ya kijiji ambayo sio imara mnaweza kujikuta mnapoteza ardhi yenu.

Mwisho kabisa naamini mabadiliko na maendeleo ya nchi hii yanaweza kuanzia kwenye ngazi ya mitaa, vitongoji au vijiji. Hii ni kwa sababu matatizo yoyote tunayokumbana nayo kama taifa yanaanzia katika ngazi ya familia na hatimaye mitaa. Kwa mfano wahalifu wote wanaishi kwenye mitaa yetu, wauzaji wa madawa ya kulevya na hata watumiaji wanakaa kwenye mitaa yetu. Hivyo tukiweza kuwa na serikali zamitaa ambazo zipo imara tunaweza kujenga misingi mizuri kama taifa.

Baada ya kuona umuhimu huo mkubwa wa serikali za mitaa sasa naomba nikushirikishe mambo matano muhimu ya kuzingatia kwenye uchaguzi huu wa serikali za mitaa.

1. Hakikisha unapiga kura na hamasisha wengine nao wapige kura.

Ule utamaduni wetu watanzania wa kutokupiga kura halafu tunakuwa wa kwanza kulalamika kwamba viongozi ni wabovu sio utaratibu mzuri. Hakikisha unapiga kura siku hiyo ya uchaguzi na pia washawishi ndugu jamaa na marafiki zako nao wapige kura siku hiyo. Kura yako moja ina thamani kubwa sana, usiidharau.

uchaguzi

2. Chagua kiongozi mwenye maono na mwenye historia nzuri.

Kwanza kabisa mtu ambaye mtamchagua awe mtu ambaye mnamjua vizuri. Awe ni mtu ambaye amekaa kwenye mtaa huo na mna historia yake nzuri ya namna ambavyo amekuwa akihamasisha mambo mbalimbali kwenye mtaa au kijiji chenu. Awe ni mtu mwenye maono na anayefikiria na kukubali mabadiliko. Kiongozi wa aina hii ataweza kushirikiana nanyi kuleta maendeleo kwenye eneo lenu.

Kujua zaidi kuhusu tabia za viongozi bonyeza maandishi haya.

3. Mtu yeyote atakayotoa rushwa usifikirie mara mbili, usimpigie kura na hamasisha wengine wasimpigie kura.

Uongozi wa serikali za mitaa ni uongozi ambao hauna manufaa makubwa kifedha zaidi ya posho ndogo ndogo. Sasa mtu ambaye anatoa rushwa lili kupata nafasi hiyo, jiulize ananufaikaje? Kwa vyovyote vile atahakikisha akipata nafasi analipa fedha yake aliyowekeza kwa kutoa rushwa hivyo atawaingiza kwenye matatizo.

4. Chagua mtu, usichague chama.

Kwa siasa zetu za Tanzania bado haturuhusu mgombea binafsi hivyo unalazimika kuchagua mgombea anayeletwa na chama fulani. Chama kinaweza kuwa na sera nzuri sana ila kama kitakuwa na mgombea ambaye hana uwezo mzuri wa uongozi sera hizo ni kazi bure. Hivyo hudhuria mikutano ya kampeni, wafatilie vizuri wagombea wote na mchague mtu ambaye unaona anaweza kuleta mabadiliko kwenye mtaa au kijiji chenu. Hata kama wewe ni mkereketwa wa chama fulani ila ukaona mgombea wa chama kingine ana sifa zaidi ya mgombea wa chama chako, mpigie kura. Mwisho wa siku maendeleo yatakuwa ni kwa mtaa wenu na sio chama chenu.

5. Tuoneshe ushirikiano na kuwawajibisha viongozi tuliowachagua.

Baada ya uchaguzi na viongozi kupatikana ni vyema kuweka tofauti za kisiasa pembeni na kupeana ushirikiano ili kiongozi mliyemchagua aweze kutekeleza majukumu yake. Kwa kuonesha ushirikiano mzuri italeta mafanikio makubwa kwa mtaa au kijiji chenu.

Pia pale ambapo kiongozi mliyemchagua anakwenda kinyume na ahadi zake ni vizuri kumwajibisha. Kwenye serikali za mitaa tupo karibu sana na viongozi wetu na hivyo ni rahisi kuhoji mambo mbalimbali ambayo mnaona hayaendi sawa.

Nichukue nafasi hii kuwatakia watanzania wote uchaguzi mwema na twende tukafanye maamuzi sahihi kwa mitaa na vijiji vyetu kwa miaka mitano ijayo.

Tanzania ni yetu sote, tushirikiane kuijenga.

Sunday, February 23, 2014

Lengo Langu Kubwa Kwenye Maisha; Kuwa Rais wa Tanzania.

  Leo nakushirikisha lengo kubwa sana kwenye maisha yangu. Lengo hilo ni kuwa rais wa nchi yangu Tanzania. Kama ilivyo kwenye kuweka lengo lolote kuna hatua muhimu za kufuata ili kuweza kufikia lengo unaloweka.   Katika lengo langu mimi ninachotaka ni kuwa rais wa nchi yangu Tanzania.

  Kwa nini nataka kuwa rais wa tanzania?

Kuna sababu nyingi zinazonisukuma kutaka kuwa rais wa nchi yangu. Hapa nitaeleza sababu chache na kadiri muda unavyokwenda nitazidi kueleza sababu nyingine.

1. Naipenda nchi yangu na ninatamani kuleta mabadiliko makubwa kwenye maisha ya wananchi na taifa kwa ujumla. Naamini nina mchango mkubwa sana kwenye mabadiliko ya nchi yangu na njia nzuri ya kutoa na kutekeleza mchango huo ni kupata nafasi kubwa kwenye uongozi wa nchi hii.

2. Naamini matatizo mengi tuliyonayo Tanzania yanaweza kutatulika kama tukiwa na viongozi ambao wana uzalendo.

3. Naamini viongozi wengi tulionao sasa hivi hawana sifa za uongozi na wengi wapo kwa maslahi binafsi hivyo wanazidi kuwa tatizo kwenye nchi yetu.

4. Naamini maendeleo ya nchi yanatokana na maendeleo ya wananchi ambao wamejengewa uwezo na sio kutokana na misaada ama mikopo.

5. Naamini mifumo mingi ni mibovu na hatuwezi kubadili nchi hii bila kubadili kabisa mifumo hiyo. Kwanza ni mfumo mzima wa uongozi, pili mfumo wa utumishi wa umma, tatu mfumo wa elimu. Mifumo hii hasa wa elimu na uongozi imekuwa kikwazo kikubwa kwetu kupata taifa ambalo linajielewa.

 

Ni lini nategemea kuwa rais wa nchi hii?

Nategemea kuwa rais wa nchi hii ifikapo mwaka 2040. Ni mbali sana lakini nina sababu za msingi za kuweka muda huo mwingi mpaka niwe raisi. Kuanzia leo mwaka 2014 mpaka kufika mwaka 2040 ni miaka 26 kuna mambo mengi sana nahitaji kuyafanya katika miaka hiyo ndio niwe rais wa Tanzania.

 

Kwa nini nimetangaza mapema na kwa nini nakuambia wewe?

1.Nimetangaza mapema na nimeweka wazi ili kupata muda wa kutosha kujiandaa. Najua kazi ya urais sio kazi lele mama, ni kazi inayohitaji busara kubwa na uwezo mkubwa wa kuamua na kutenda. Hivyo kwa miaka 26 ijayo nitajifunza mambo mengi sana ya uongozi ili niwe kiongozi bora na ninayejua ni kitu gani ninafanya.

2. Nataka nijue ni watu gani ninaoweza kufanya nao kazi. Kama rais wa nchi nitahitaji wasaidizi ambao nitawachagua mimi. Nitakapokuwa rais nitatumia vigezo vikali sana kuchagua watu watakaoshika sehemu za uongozi. Sitotumia kujuana au urafiki, nitatumia uwezo wa mtu. Naamini kwenye miaka hii 26 nitakutana na watu wengi na nitaweza kupima uwezo wao hasa kwenye matendo. Kama wewe ni rafiki yangu na unasoma hapa ni vyema ukawa unaonesha uwezo wako kwenye mambo yako binafsi unayofanya. Hata kama tumewahi kulala kitanda kimoja usishangae ukija kukosa nafasi hata ndogo sana wakati nitapokuwa rais.

3. Nahitaji mchango wako ili niweze kuwa kiongozi bora. Nahitaji ushauri wako, na nahitaji kupingwa ninapotoa hoja ambazo haziendani na mahitaji yetu. Naamini haya yote yatanijenga kuwa kiongozi bora.

 

Kwa sasa nitatumia blog hii kama sehemu ya kujifunza uongozi. Nakukaribisha twende pamoja kama na wewe una ndoto ya kuwa kiongozi kwenye maisha yako. Kila siku ya jumapili nitakuwa naweka makala moja inayohusisha UONGOZI, SIASA AU RAIS KIVULI. Pia nitakuwa nashirikisha watu vitabu mbalimbali vya uongozi nitakavyokuwa navisoma.

Karibu tujiandae kulijenga taifa letu.

Nategemea maoni yako hapo chini.