Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Sunday, March 16, 2014

Sifa Moja Muhimu Ambayo Kila Kiongozi Mkubwa Anayo.

Kwenye makala zilizopita tuliona ni muhimu kwa kila mmoja wetu kuwa kiongozi kwenye maisha yake na shughuli anazofanya. Pia tuliona kwamba kila mmoja wetu anaweza kuwa kiongozi kama ataamua, iwe kwa kuendeleza sifa za uongozi zilizopo ndani yake au kwa kujifunza sifa za uongozi.

Leo tutaangalia sifa moja muhimu ambayo kila kiongozi mkubwa anayo na imechangia sana kwenye mafanikio yao kiuongozi. Ninaposema viongozi wakubwa simaanishi viongozi walioshika nafasi kubwa bali viongozi ambao wamefanya mambo makubwa ambayo yameleta mabadiliko kwa watu wengi na dunia kwa ujumla. Viongozi kama Nyerere, Mandela na hata viongozi wakubwa kwenye nyanja za biashara na kazi wameweza kufikia mafanikio makubwa kutokana na sifa hii moja.

Kwa kuwa na wewe unataka kuwa kiongozi wa maisha yako, kiongozi kwenye familia yako, kiongozi kwenye kazi au biashara zako na hata kiongozi wa kuwakilisha watu ni vyema ukaijua sifa hii na kuanza kujifunza au kuiendeleza ili uweze kufikia malengo yako. Sifa hii moja sio kwamba ndio inakutosha kuwa kiongozi ila kwa kuwa na sifa hii unaweza kuziendeleza sifa nyingine za uongozi. Kwa kukosa sifa hii ni vigumu kuweza kuzitumia sifa nyingine za uongozi ulizonazo.

Sifa muhimu ya uongozi ninayozungumzia hapa ni ujasiri. Ujasiri ni sifa ambayo imewawezesha viongozi wakubwa kufanya mambo makubwa kwenye uongozi wao. Kukosa ujasiri ndio kumefanya watu wengi washindwe kwenye uongozi.

Kuweza kusimamia kile unachoamini ni sahihi hata kama watu wengi wanakupinga kunahitaji ujasiri wa hali ya juu. Kama ilivyotokea kwa Mandela, alikuwa na ujasiri wa kuweza kusimama na kupinga ubaguzi hata baada ya kufungwa jela miaka 27. Wafanyabiashara wakubwa na waliofanikiwa sana mwanzoni walipingwa, kukatishwa tamaa na hata kuchekwa kwamba mawazo yao ya biashara hayawezi kufanikiwa. Ila kutokana na ujasiri waliweza kuendelea na misimamo yao na baadae ikawa historia kubwa ya mabadiliko.

Inahitaji ujasiri wa hali ya juu kuenda tofauti na watu wengine ili kufuata ndoto zako. Inahitaji ujasiri mkubwa kuweza kufanya kazi na watu ambao wana misimamo tofauti na wewe na mkaweza kuelewana. Inahitaji ujasiri mkubwa kufanya na kusimamia maamuzi magumu ambayo wengi hawayafurahii ila yana manufaa kwao baadae. Yote haya yameweza kutengeneza viongozi wakubwa sana na walioshindwa ujasiri wa kufanya mambo haya wameishia kuwa kawaida tu.

Kutokukata tamaa wakati umeshindwa, kuweza kusimama baada ya kupata hasara kubwa na kutokuwasikiliza wanaokukatisha tamaa ni muhimu sana kwenye mafanikio ya kibiashara na kikazi. Watu wenye ujasiri wanaweza kuvuka changamoto hizo na kuwa viongozi wa mfano kwenye kazi na biashara zao.

Unaweza kujifunza ujasiri?

Huenda mpaka kufika hapa umeshaona kwamba ujasiri kwako ni kitu kigumu sana hivyo njia yako ya kuwa kiongozi imeshakutana na kizuizi kikubwa. Habari njema kwako ni kwamba unaweza kujifunza ujasiri. Unawezaje kujifunza ujasiri?

Ili uwe na ujasiri kitu cha kwanza kabisa ni lazima ujue ni nini unasimamia. Kama huna kitu unachosimamia utakubaliana na kila kitu na kama unakubaliana na kila kitu wewe sio jasiri na huwezi kupata mafanikio makubwa kwenye jambo lolote unalofanya, hilo halina ubishi. Jua ni kitu gani unasimamia, jua ni kwa nini unasimamia na jua ni nini unategemea kutoka kwenye huo msimamo wako. Hii ni kwenye maisha, familia, kazi, biashara na hata uongozi wa wananchi.

Baada ya kujua unachosimamia izidi hofu. Hofu na woga ndio vitu vinavyoondoa ujasiri kwa watu wengi. Ukiweza kuishinda hofu utaweza kukamilisha mambo mengi sana kwenye maisha yako na kuacha alama. Kama utakubaliana na hofu na kuacha kufanya mipango yako hakuna kitu kikubwa utakachofanya. Watu wenye ujasiri na waliofanikiwa sio kwamba hawana hofu ila wamechagua kuzishinda hofu zao. Chagua na wewe kushinda hofu zako na kufanya yale unayojua ni sahihi na yatawasaidia watu wengine.

Kuna faida kubwa ya kuwa na ujasiri kwenye maisha yako. Watu wenye ujasiri huwavutia watu wengine kuwa karibu nao na hivyo kuangaliwa kama kiongozi. Watu wenye ujasiri hufanya mambo makubwa na kuwafaidisha wengine hivyo wengine kutaka kufanya kama wao. Hivi ndivyo ujasiri unajenga viongozi wakubwa. Na kwa kuwa wewe unataka kuwa kiongozi mkubwa anza kwa kujenga ujasiri wako.

Kwanzia wiki ijayo tutazijadili sifa 21 za kiongozi kutoka kwenye kitabu  The 21 Indispensable Qualities of a Leader. Tutajadili sifa tatu tatu mpaka zitakapoisha. Kuhakikisha hukosi makala hizi nzuri za uongozi weka email yako hapo juu kwenye blog sehemu iliyoandikwa jiunge hapa kupata makala mpya inapotoka

Pia usiache kupitia blog hii kila jumapili ili kujifunza mengi kuhusiana na uongozi. Washirikishe marafiki zako nao ili wajifunze masomo haya ya uongozi. Pia weka maoni yako hapo chini kuhusiana na mambo ya uongozi.

Tafadhali Washirikishe Wengine Makala Hii Nzuri!
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →
Powered By: BloggerYard.Com

0 comments:

Post a Comment