Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Sunday, March 9, 2014

Kiongozi Anazaliwa au Anatengenezwa? Jibu Hili Hapa.

Kumekuwa na mjadala au mabishano kwa muda mrefu ikiwa kiongozi anazaliwa au anatengenezwa. Wapo wengi ambao wanaamini watu wenye sifa za uongozi wanazaliwa nazo na haziwezi kutengenezwa. Wapo wengine wanaoamini viongozi wanatengenezwa kutokana na jamii wanayoishi na elimu wanayopata.

Nani yupo sahihi hapa? Je wewe una maoni gani juu ya tabia za uongozi? Je mtu anazaliwa nazo au anazipata kutoka kwenye malezi na elimu?

Majibu yote mawili ya kiongozi kuzaliwa au kutengenezwa yapo sahihi kabisa. Ni kweli kwamba kuna watu wanazaliwa wakiwa na sifa za uongozi na kuna wengine wanajifunza uongozi kutokana na malezi na elimu wanayopata.

Kwa nini tuna upungufu mkubwa wa viongozi?

Pamoja na kwamba viongozi wanaweza kuzaliwa na wengine kutengenezwa bado tuna upungufu mkubwa sana wa viongozi kwenye jamii zetu. Hii inasababishwa na kwamba jamii haitengenezi viongozi. Hivyo viongozi pekee wanaopatikana ni wale waliozaliwa na sifa za uongozi na huwa ni wachache sana.

Mfumo wa maisha wa jamii nyingi hautengenezi viongozi. Watoto wanakuzwa bila ya kujengewa misingi ambayo inawasaidia kuweza kufanya maamuzi kama viongozi. Jamii nyingi zinalea watoto kwa kuwaepusha wasikutane na changamoto ambazo zinawafanya wafikiri zaidi. Kwa njia hii jamii sio tu kwamba haitengenezi viongozi bali inaua sifa za uongozi kwa baadhi ya watoto waliozaliwa nazo. Kwenye jamii kuna watu wengi sana ambao hawana sifa za uongozi, kwa kuwa watoto wanaiga tabia za wanaowazunguka ni rahisi sana kwao kufanana na wanajamii ambao hawana sifa za uongozi.

Kitu kingine kikubwa kinachoua uongozi ni mfumo wa elimu. Mfumo wa elimu hasa kwa nchi yetu Tanzania haujakaa kutengeneza viongozi. Kwanzia darasa la kwanza mpaka elimu ya chuo mtoto anafundishwa kukazania vitu vichache ili kufaulu masomo. Hapewi nafasi ya kufikiri tofauti na kuibua na kupambana na changamoto. Pia mfumo wa elimu unajenga watu kuwa na ubinafsi na kufikiria maisha yao tu badala ya kufikiri na ya wale wanaomzunguka. Kwa njia hii mfumo wa elimu unashindwa kutengeneza viongozi na inaua sifa za uongozi kwa baadhi ya wenye nazo.

Hata wewe unaweza kuwa kiongozi.

Hata wewe unaweza kuwa kiongozi, iwe umezaliwa na sifa za uongozi ama hukuzaliwa nazo. Unaweza kufufua sifa za uongozi zilizokufa ndani yako au kujifunza sifa mpya za uongozi.

Kama nilivyosema kwenye makala iliyopita ni muhimu sana wewe kuwa kiongozi(kuisoma bonyeza hapa). Ni muhimu wewe kuwa kiongozi kwa sababu wote wanaofanikiwa kwenye chochote wanachofanya wanasifa za uongozi. Ili uweze kufanikiwa kwenye biashara, kazi, sanaa, michezo na hata uongozi wa kisiasa ni lazima uwe na sifa za uongozi. Hata kwenye malezi ya familia, wazazi wenye sifa za uongozi wanalea familia zao vizuri na kuwa na watoto wanaoweza kuendesha maisha yao vizuri.

Hata wewe unaweza kuwa kiongozi mzuri na ukafanikiwa sana kwenye shughuli zako. Unaweza kujifunza sifa na tabia za uongozi na ukaanza kuzitumia kwa mafanikio yako. Kuna vitabu na maandiko mengi sana yanayozungumzia uongozi. Unaweza kutafuta na kuanza kusoma, ila kama unaona huna muda wa kutosha unaweza kuwa unajifunza kupitia blog hii. Kila wiki kutakuwa na makala moja inayohusiana na uongozi hivyo unaweza kuwa unakuja kujifunza hapa. Pia ili kuhakikisha hukosi makala yoyote inayohusiana na uongozi au mengineyo weka jina na email yako hapo juu kwenye blog na utapata makala hizi moja kwa moja kwenye email yako.

Karibu tutengeneze viongozi wa kuliinua taifa letu kijamii, kisiasa, kiuchumi na kimaendeleo kwa ujumla. Hili ni jukumu letu sote.

Tafadhali Washirikishe Wengine Makala Hii Nzuri!
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →
Powered By: BloggerYard.Com

1 comments: