Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Sunday, April 6, 2014

Siri Kumi za Mafanikio Kwenye Uongozi.

Katika watu wengi wanaopewa nafasi za kuongoza kuna wachache sana ambao wanakuwa ni viongozi bora. Wengine wanaishia kuwa tu na majina ya uongozi ila wanashindwa kufanya mambo makubwa kupitia nafasi zao za uongozi.

Mpaka unasoma hapa naamini unataka kuwa kiongozi bora. Ili uweze kupata mafanikio kwenye uongozi, kuna tabia kumi muhimu unatakiwa kuwa nazo na kuziendeleza. Tabia hizo ziko wazi kabisa ila kutokana na watu wengi kutozipa mkazo zimegeuka na kuwa siri kubwa.

Leo tutazungumzia tabia kumi muhimu za kufanikiwa kwenye uongozi. Tabia hizi zinafanya kazi bila ya kujali wewe ni kiongozi wa aina gani. Uwe ni kiongozi usiyekuwa na cheo, kiongozi wa wananchi, kiongozi wa shughuli zako au hata kiongozi wa maisha yako ni vyema ukaanza kutengeneza na kuendeleza tabia hizi.

1. Mfano.

Ili uweze kufanikiwa kama kiongozi ni lazima uwe mfano bora kwa wale unaowaongoza. Utatengeneza mfano mzuri pale ambapo utakuwa unatenda yale unayohubiri. Lazima wewe uwe wa kwanza kuonesha mwendo ili wafuasi wako nao wafuate. Ile kauli kwamba “fuata maneno yangu, usifuate matendo yangu” imesababisha watu wengi sana kushindwa kwenye uongozi. Watu wanapenda kumfuata na kumheshimu mtu ambae anaonesha mfano wa vitendo kwao.

2. Nguvu,

Mafanikio katika uongozi yanategemea sana nguvu ya kiongozi. Naposema nguvu simaanishi nguvu za kimwili pekee bali hata nguvu za kihisia, nguvu za kiakili na nguvu za kiimani. Kiongozi unapokuwa na nguvu hizi inakuwa rahisi kuzitoa kwa wale unaowaongoza.

3. Shauku.

Viongozi wanaofanikiwa sana ni wale wenye shauku kubwa kwenye kazi zao na kwenye maendeleo ya watu wanaowaongoza. Kwa kuwa na shauku kunawafanya wafanye mambo bora zaidi. Pia shauku inaambukizwa mpaka kwa wafuasi.

4. Uvumilivu.

Bila ya uvumilivu huwezi kuwa kiongozi bora, hakuna zaidi ya hapo. Viongozi wengi waliofanikiwa sana walipitia mambo magumu sana kwenye maisha yao. Hata wewe utapitia mambo magumu sana kwenye uongozi wako na maisha yako kwa ujumla. Kuna wakati utashindwa, kuna wakati utakosea sana, tumia nyakati hizi ngumu kujijenga na kuwa imara. Unapovumilia na kuvuka nyakati hizi ngumu unatoa imani kubwa kwa wafuasi wako.

5. Uelewa wa kihisia.

Hisia ni moja ya vitu vinavyoweza kumjenga kiongozi au kumbomoa ndani ya muda mfupi sana. Ili kuwa kiongozi bora ni lazima uzijue hisia zako na ujue ni jinsi gani ya kuzimiliki. Usikubali hisia zako zikutawale mwishowe uanze kufanya mambo yatakayoharibu sifa zako. Pia ni muhimu kuweza kusikiliza na kuelewa hisia za wafuasi wako na kuweza kuwasaidia kupata mtazamo sahihi.

6. Uwezeshaji.

Kiongozi bora ni yule anayewawezesha wafuasi wake kuchukua hatua na kufanya mabadiliko kwenye kazi zao na maisha yao. Katika uwezeshaji kiongozi anawapa watu nguvu na mamlaka ya kufanya mambo ambayo yatakuwa na manufaa kwenye maisha yao. Unapowawezesha watu kuchukua hatua, unawajengea ujasiri ambao baadae utawapelekea kuwa viongozi bora.

7. Ufanisi.

Viongozi bora huwa na ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu yao. Katika ufanisi viongozi huwa na mipango mizuri ambayo itawasaidia kufikia malengo waliyojiwekea. Viongozi bora hufanya jambo sahihi na sio kufanya jambo kwa usahihi. Uongozi bora unapimwa kutokana na majibu anayozalisha kiongozi na sio kwa hotuba nzuri.

8. Kuchukua hatua.

Viongozi bora wanajua ni wapi walipo na pia wanajua ni wapi wanataka kwenda na huchukua hatua mara moja ili kufika wanakotaka kwenda. Hapa ndipo viongozi wanapobadili maono kuwa uhalisia. Kama kiongozi una ahadi na maneno mengi mazuri ila huwezi kuchukua hatua ya kuyatekeleza hufai kuwa kiongozi bali muigizaji.

9. Mafanikio.

Mafanikio ni nguzo muhimu sana kwa viongozi waliofanikiwa. Kiongozi lazima awe amefanikiwa kwenye shughuli zake ili aweze kupata wafuasi wanaotaka kufanikiwa kama yeye. Viongozi bora hupanga kuwa bora kwenye shughuli zao na hivyo kukazana kila siku kutoa majibu yenye ubora.

10. Maadili.

Tabia hii imekuja mwisho ila ilipaswa kuwa ya kwanza kabisa. Huwezi kufanikiwa kwenye uongozi wa aina yeyote ile kama huna maadili. Watu wanapenda kumfuata mtu ambaye anajiheshimu na hivyo kuamini atawaheshimu. Kama kiongozi una skendo chafu ni vigumu sana watu kukupa imani ya kweli kutoka ndani ya mioyo yao. Tatizo kubwa tunalolipata kwenye uongozi hapa Tanzania ni maadili mabovu ya viongozi. Kuwa kiongozi wa mfano kwa kuwa na maadili mazuri kwenye maisha yako.

Kwa kujijengea na kuendeleza sifa hizo kumi utajijenga kama kiongozi wa mfano na mwenye mafanikio makubwa sana. Kumbuka wewe ni kiongozi, hivyo endeleza uongozi wako ili uweze kuwasaidia watu wengi zaidi.

Kama una jambo lolote unaona ni zuri kutushirikisha tafadhali weka maoni yako hapo chini. Kwa kuweka maoni yako hapo chini ni dalili nzuri kwamba unaelekea kuwa kiongozi bora na wa mfano.

Karibu kiongozi tujadiliane yaliyo mema kwenye uongozi.

Tafadhali Washirikishe Wengine Makala Hii Nzuri!
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →
Powered By: BloggerYard.Com

0 comments:

Post a Comment