Jiunge Hapa Kupata Makala Mpya Inapotoka!

We'll not spam mate! We promise.

Sunday, April 20, 2014

Dalili Kumi Kwamba Tayari Wewe Ni Kiongozi.

Kwenye makala zilizopita tumeona ni muhimu sana kwa kila mmoja wetu kuwa kiongozi. Pamoja na umuhimu huo sio watu wote ni viongozi na sio watu wote wataweza kuwa viongozi. Na hata ambao ni viongozi sio wote ni viongozi bora wanaotoa matokeo mazuri.

Pia tumejifunza kwamba kiongozi anaweza kuzaliwa au kutengenezwa. Kutegemea na mazingira na uhitaji wa mtu, mtu yeyote anaweza kuendeleza tabia za uongozi ndani yake.

Leo tutaona dalili kumi za sifa ya uongozi. Kama wewe una sifa hizi tayari wewe ni kiongozi na unahitaji kujiendeleza zaidi ili kuweza kufanya makubwa zaidi kwenye uongozi wako. Kama huna dalili hizi kuna habari nzuri na mbaya kwako.

Habari mbaya kwako ni kwamba utaendelea kuwa mfuasi maisha yako yote na kwa nafasi kubwa utashindwa kuonesha uwezo wako wa kweli na kuleta tofauti kubwa kwenye jamii yako na dunia kwa ujumla.

Habari nzuri ni kwamba unaweza kujifunza tabia hizi na ukawa kiongozi bora sana. Uzuri ni kwamba kila kitu unaweza kujifunza, ni utayari wako na juhudi zako ndivyo vitakufanya uweze kujua kile unachotaka kujua. Njia bora ya kujifunza uongozi ni kujua vitu na kuvifanyia kazi. Hutakuwa kiongozi kwa kusoma tu hapa, bali soma na utumie yale unayojifunza kwenye maisha yako ya kila siku.

Kwa kifupi sana naomba nitaje dalili kumi zinazoonesha kwamba wewe ni kiongozi. Kwa maelezo zaidi tunaweza kujadiliana kwenye maoni hapo chini.

1. Unapenda kuleta mabadiliko.

2. Una ndoto kubwa sana mpaka wengine wanaona haziwezekani.

3. Husubiri kuambiwa nini cha kufanya,

4. Unapenda kutatua matatizo yanayowasumbua wengine.

5. Hupendi kulalamika au kulaumu wengine.

6. Unajali sana na kukuza mahusiano.

7. Matendo yako na maneno yako vinaendana.

8. Hukubaliani na mifumo isiyo na tija.

9. Uko tayari kukiri makosa na kuomba radhi.

10. Unapenda kujifunza mambo mapya na kuhusu uongozi.

Kama una dalili hizo kumi hongera wewe ni kiongozi. Kama huna usikate tamaa bado una nafasi kubwa ya kujijengea uongozi.

Uongozi unaanza na kuchagua kuwa kiongozi, baada ya hapo unaendelea kujifunza na kupata uzoefu. Karibu kwenye mafunzo ya kuongozi kupitia blog hii. Ili kuhakikisha hukosi mafunzo haya weka email yako hapo juu kwenye blog ili upate makala hizi moja kwa moja kwenye email yako.

TUKO PAMOJA.

Tafadhali Washirikishe Wengine Makala Hii Nzuri!
SOCIALIZE IT →
FOLLOW US →
SHARE IT →
Powered By: BloggerYard.Com

0 comments:

Post a Comment